Tafuta/Search This Blog

Monday, May 9, 2011

Mkapa aibuka shujaa.

BAADA ya kimya cha muda mrefu, huku akizongwa na kutuhumiwa kwa mambo kadhaa, Rais mstaafu Benjamin Mkapa ameibuka shujaa katika siku za karibuni. Hata mwenyewe amelitambua na kulithibitisha hilo.

Kuzingatia vipaumbele, kuinua uchumi na kukusanya kodi, ni baadhi ya mambo anayojivunia, na ambayo jamii inayatumia kumpima na kulinganisha utawala wake na wa Rais Jakaya Kikwete.

Mkapa ambaye mara baada ya kumaliza ngwe ya uongozi wake aliandamwa na kashfa za ufisadi, hivi sasa anatajwa kuwa kiongozi mahiri aliyemudu kudhibiti mfumuko wa bei pamoja na kukuza uchumi, tofauti na utawala wa sasa wa Rais Kikwete.

Utawala wa sasa umekuwa ukilalamikiwa kwa kufifisha uchumi, kushindwa kudhibiti mfumuko wa bei pamoja na maisha ya wananchi kuzidi kuwa magumu kadiri siku zinavyosonga mbele.

Serikali ya Awamu ya Nne ilipoingia madarakani mwaka 2005, zilifanyika jitihada za chinichini kubeza kazi za Rais Mkapa na kuibua kashfa mbalimbali zilizowahusu watendaji wake na yeye mwenyewe.

Kuna wakati wananchi walifikia mahali pa kuaminishwa kwamba Rais Mkapa aliharibu nchi, hata baadhi ya vijana wakadiriki kumzomea.

Hata hivyo, ugumu wa maisha, kinyume cha ahadi ya maisha bora ya Rais Jakaya Kikwete, umewafanya wananchi wamwone Rais Mkapa kama shujaa aliyeinua uchumi, ambao sasa hivi unadidimia na maisha yanakuwa magumu zaidi.

Kiongozi huyo ambaye mara nyingi amekuwa kimya kuzungumzia masuala mbalimbali ya utawala wake, alionyesha wazi hisia zake juzi usiku jijini Dar es Salaam baada ya kukabidhiwa tuzo ya heshima kwa mchango wake wa kuthamini michezo nchini, iliyoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA).

Serikali ya Mkapa ndiyo iliyosimamia ujenzi wa Uwanja wa Taifa kwa ushirikiano na China. Ni uwanja wa kisasa wenye uwezo wa kuingiza watu 60,000 waliokaa.

Mkapa alisema wakati akiingia madarakani aliikuta nchi katika hali ngumu ya kiuchumi, jambo lililomfanya kuweka kando mambo mengi na kutoa kipaumbele katika uchumi ili wananchi waweze kupata unafuu wa maisha.

Alibainisha kuwa alijikita katika uboreshaji wa ukusanyaji wa kodi na kulipa madeni ili kuliokoa taifa na wananchi wake kwenye hatari ya kudidimia kiuchumi.

Alisema kazi ya kuimarisha uchumi haikuwa nyepesi, hivyo alilazimika mara kadhaa kuumiza kichwa na kukubaliana na washauri wake wakiwemo mawaziri katika kipaumbele cha kuimarisha uchumi wa nchi.

Mkapa alisema kutokana na mazingira aliyoyakuta wakati anaingia madarakani alilazimika kutumia kanuni za hayati Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere za kuwa kupanga ni kuchagua na kutenda ni kuamua.

“Mwalimu Nyerere alikuwa akisisitiza umuhimu wa kufanya jambo husika kulingana na wakati uliopo, nami nilipanga, nikachagua na matokeo yake yakaonekana,” alisema.

Alisema kuwa aliona ni muhimu kujenga misingi imara ya uchumi kwa kuimarisha ukusanyaji wa kodi ili kuiondoa nchi katika wimbi kubwa la madeni iliyokuwa ikidaiwa.

“Katika kipindi changu cha awamu ya kwanza nilipoingia madarakani, nilionekana kutopenda michezo kwa sababu nililazimika kuongoza kiukapa kutokana na mazingira niliyoyakuta. Hivyo, niliamua kuanza na kuimarisha uchumi kwa kujenga misingi ya kukusanya kodi.

“Pamoja na mambo mengine, kazi hiyo ilifanyika kwa umakini mkubwa na ilinifanya nishindwe kuhudhuria hata masuala ya michezo… na hiyo ikawa sifa yangu ya kuonekana sipendi michezo,” alisema.

Aliongeza kuwa mazingira ya wakati ule yalimfanya afikirie zaidi uchumi na aliiwezesha serikali yake kupata msamaha wa madeni iliyokuwa ikidaiwa na nchi wahisani na wafadhili.

Mkapa alisema baada ya awamu ya kwanza kuimarisha uchumi ilipofika awamu ya pili ya utawala wake ndipo sasa akaamua kugeukia mambo mengine, yakiwemo hayo ya michezo ambapo aliona kitu pekee ambacho anaweza kuwaachia Watanzania na kuwa kumbukumbu nzuri kwake ni kujenga uwanja wa soka wa kimataifa katika Jiji la Dar es Salaam.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali wakiongozwa na Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Emmanuel Nchimbi na watu mashuhuri ambao baadhi yao wamelilitumikia taifa katika nyanja mbalimbali.

Mkapa pamoja na kupewa heshima hiyo bado alitoa wito kwa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini (TASWA) kuhakikisha wanautambua mchango wa Rais Kikwete katika medani ya michezo.

Alisema kujengwa kwa uwanja huo wa kimataifa Rais Kikwete amefanya kazi kubwa ya kujenga hoja wakati walipokwenda China kuomba msaada wao ili kufanikisha ujenzi huo.

Alisema kuwa baada ya serikali yake kuamua kujenga uwanja wa mpira wa miguu wa kimataifa, kazi ya kujenga hoja na kufanya mazungumzo ya namna gani uwanja utakuwa alimuachia Rais Kikwete wakati huo akiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na hatimaye hoja zake kufanikiwa na China kukubali kuujenga.

“Hivyo Rais Kikwete anastahili heshima ya kutambulika kwa mchango wake katika michezo kwa kitendo chake cha kuwezesha kujengwa uwanja huo pamoja na aliyekuwa Waziri wa Kazi, Ajira na Vijana, Profesa Juma Kapuya, kutokana na kuhimiza mara kwa mara kuhusu mchakato wa kuanza kwa ujenzi wetu,” alisema Mkapa.

“Kapuya amefanya kazi kubwa katika kufanikisha serikali kujenga uwanja huo wa kimataifa, alikuwa akinihimiza mara kwa mara na hatimaye tukafanikisha. Hivyo TASWA mnapaswa kutambua mchango wake na ikiwezekana naye apewe tuzo ya heshima,” alisema.

Aliwaomba Watanzania kutambua haki na wajibu wa kuutunza uwanja huo ili uweze kudumu kwa muda mrefu na hatimaye kuwa kumbukumbu hata kwa kizazi kinachokuja.

Wakati akizungumza hayo, alikuwa akiwaeleza waliofika kushuhudia tukio hilo la utoaji wa tuzo kwa mwanamichezo bora wa mwaka 2010.

Katika hafla hiyo, Mkapa alionekana kukonga nyoyo za waliohudhuria ambapo mara kwa mara alilazimika kusitisha kwa muda kusoma hotuba yake kutokana na kushangiliwa, ikiwa ni ishara ya kuukubali utawala wake na mambo aliyolifanyia taifa.

Akizungumza katika sherehe hizo, kabla ya kutoa tuzo ya mwanamichezo bora, mgeni rasmi Makamu wa Rais, Dk. Mohamed Gharib Bilal, alisema amefanya kazi na Rais Mkapa wakati huo yeye akiwa Katibu Mkuu Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, ambapo alisifu ujasiri aliokuwa nao Mkapa katika mambo mbalimbali.

“Rais wetu mstaafu tunakupa heshima kubwa ya kutambua kuwa nchi yetu inahitaji kufungua njia katika sekta ya michezo na kwa kufanya hivyo ulikubali kubana bajeti ya serikali ambayo ingejenga zahanati na shule lakini ukatambua afya njema na elimu bora hupatikana kama wananchi wanashiriki michezo.

“Uwanja uliotuachia ni kielelezo tosha na wala usikatishwe tamaa na vijana hawa wanaposhindwa kutupa matokeo mazuri katika mechi zao na hakika kazi yako uliyofanya itabaki katika ramani ya michezo nchini na kamwe haitasahulika,” alisema Dk. Bilal huku akisifu ujasiri wa rais ambao alithubutu na hata kuweza kujenga uwanja huo wa kimataifa.

-Tanzania Daima.

No comments: