Tafuta/Search This Blog

Tuesday, March 7, 2017

RAIS MAGUFULI ANATUTAKA TUSOME KITABU CHA DONALD TRUMP




The beginning of every government starts with the education of our youth.
(Mwanzo wa kila serikali unaanza na kuwapatia elimu vijana wetu)
—Pythagoras


Katika kitabu chake cha “Think Like a Champion” yaani fikiria kama mshindi, mwandishi Donald J. Trump ambae kwa sasa ni Rais na Amri Jeshi mkuu wa taifa tajiri na nguvu za kijeshi la Marekani, amenukuu falsafa ya Pythagoras.


Muandishi Donald Trump, amehimiza umuhimu kwa kujifunza na kuoanisha aina ya kujifunza kama mwanzo mpya kwenye kila zama ambayo mtu unaingia. Katika kitabu hicho Donald Trump ameonesha jinsi Pythagoras aliekuwa nguli wa falsafa hususani katika somo la hisabati, mara nyingi alitafsiri mambo mengi kwa kuoanisha au kuwakilisha na tarakimu au nambari.


Donald Trump yeye kama mfanya biashara nyakati ameandika na kupiga chapa kitabu kicho yaani mwaka 2009 ameonesha kuwa kuna muunganiko wa moja kwa moja kati ya elimu inayompa mtu mmoja mmoja maarifa hali kadhalika jamii nzima kupata maarifa kupitia mifumo mbalimbali ya elimu.


Mie ninaendika makala hii kwa uzoefu na ujuzi niliopata wakati nasoma chuo cha ualimu na baadae kupata mafunzo ya taaluma nyingine, naweza kurejea jambo ambao nimewahi kuandika huko nyuma kuwa sisi wanadamu, tuna namna ya kujifunza shule au vyuoni (formal education), kuna namna ya tunajifunza kwa malengo maalum ili kupata ujuzi tunaoutaka (non-formal education). Vilevile tunaweza kujifunza kwa kupitia vitabu, majarida, mitandao ya kijamii, program za radio, televiseni n.k na hii inaitwa (informal education). Vyovyote vile, maarifa tunayoyapata yanatakiwa kutubadilisha namna ya kufikiri na kuzalisha mabadiliko ya kitabia.


Trump, alijikita katika kusisitiza kila mtu anapoanza jambo jipya, kuna umuhimu wa kujifunza au kujiongezea maarifa mapya kuhusiana na mambo mapya anayotaka kuyafanya. Mwandishi ambae ni Rais wa awamu ya 45 kwa sasa ya Marekani amejielezea kwa uzuri namna ambavyo amekuwa katika kujifunza ujenzi wa nyumba na hoteli ili anapokuwa na wahandisi-wajenzi walau asiachwe nyuma na lugha za kimsingi za kiufundi hasa katika ujenzi.


Kuna nyakati alijikita katika uendelezaji wa viwanja vya gofu, ilimlamlazimu pia atafute kundi la wataalamu wa kucheza mchezo wa gofu na wajenzi wa viwanja wa gofu. Lengo lake, ilikuwa ni kukaa na wataalamu kwa lengo la kupata taarifa za msingi kutoka kwenye uzoefu wa sekta au biashara ambayo alikusudia kuifanya.


Donald Trump aliamini na anaamini sana katika hisia mpya huwa zinajengwa katika misingi ya mwanzo mpya na mwanzo mpya umeunganishwa na maarifa mapya yanayopelekea namna mpya ya kufikiri na namna mpya ya kutenda ili kupata matokeo mapya.


Haina tofauti na msemo wa kibiblia wa umuhimu wa divai mpya katika chupa mpya ili kupata matokeo tarajiwa. Tofauti na divai mpya unaweka katika chupa ya zamani. Inapelekea kupoteza divai na chupa hali kadhalika.


Natamani kununua au kuazima uzoefu wa falsafa ya Donald Trump katika muktadha wa Tanzania ya Rais John Pombe Magufuli na Watanzania walio wengi.


Kuna namna Mheshimiwa Rais ameingia darasani kama mwalimu na anatoa mafunzo kwa chaki ubaoni. Wakati Mwl. Magufuli anafundisha kwa mujibu wa mungozo mpya wa somo (new syllabus) kwa upande mwingine wanafunzi ambao ni Watanzania wanakumbuka mafunzo na malezi ya Mwl. Jakaya Mrisho Kikwete ya awamu ya 4. Na wengi wakitaka kuishi kama awamu ya 4.


Falsafa ya Mwl. Kikwete ilikuwa 1+ ( ) = 5. Wanafunzi ambao ni Watanzania tulikuwa na jukumu la kufikiri ni namba ngapi ikijumlishwa na moja tunapata 5. Kwa muongozo wa kujifunza haukuhitaji njia ya kuonesha jibu ambalo ni 4 umelipataje. Na kwa muongozo wa mafunzo yale, ukiweka 4 mwalimu atakupa vema kwa kuwa jibu ililoweka ni sahihi.


Mara hii ameingia Mwl. Magufuli ambae ana swali kama lile la mwalimu wa awamu ya nne, isipokuwa badala ya parandesi, wakati swali lina herufi X
1+X = 5.


Mwalimu Magufuli anataka utafute thamani ya X kwa njia za kihisabati za jiometri.


Sote tunakubaliana kuwa thamani ya X ni 4, isipokuwa njia ya kuifikia 4 ni tofauti na muongozo wa mafunzo ya Mwl. Kikwete.


Awamu ya 5 anatutaka ili kupata jibu, sisi Watanzania ambao ni wanafunzi darasani, tuna wajibu wa kujua kwamba tunatakiwa kuonesha njia ya kulifikia jibu ambalo ni 4.


Kwa lugha rahisi inatakiwa kuchukua swali 1+X = 5 na kutoa 1 kila upande


1+ (-1)+ X = 5 – 1


Jibu litakalopatikana litakuwa wazi kabisa kuwa


0 + X = 4


Hivyo basi kumbe thamani ya X = 4.


Huu ndiyo mfumo wa muongozo wa mafunzo anayotumia mwalimu wa awamu ya 5. Kuna uwezekano kutokana na wepesi wa masomo awamu ya 4, kuna nyakati mwalimu alihitaji tuimbe nyimbo kama sehemu ya kujifunza.


Isipokuwa muongozo wa kujifunza na kufundishia uliopo sasa watutaka tujue namna tofauti ya kutafuta thamani ya X. Muongozo wa mwalimu hautupi fursa ya kuimba kama namna ya kujifunza kama kule nyuma. Na hapa ndipo tofauti inapoanza kuonekana kwani baadhi ya wanafunzi bado wanatamani uji kumbe tupo katika zama za kula ugali na nyama ya mifupa. Tunawajibika kutumia meno yetu kutafuna kuitoa nyama katika mifupa.


Wanafunzi darasani (yaani Watanzania wengi) bado wanataka mwl. Magufuli afundishe kama mwl. Kikwete na kutumia njia za zamani kuja na jibu la thamani ya X.


Nitoe rai kwa Watanzania wenzangu ambao ni wanafunzi katika darasa la mwalimu wa awamu ya 5; chonde chonde, tuna jukumu moja kubwa la kufanywa upya namna ya kufikiri. Namna pekee ya kufikiri na kukubaliana na ukweli, mfumo mpya wa muongozo wa mafunzo ndivyo unavyotaka, na mwalimu tulie nae, muongozo wa masomo na mbinu zake za kujifunzia si kuimba (nibebe nibembeleze kama wimbo mmoja uliowahi kutamba katika nyimbo za injili).


Tukiji-position kwa kujua tupo awamu ya 5 na kuamua kujikita katika mbinu mpya za kukokotoa ili kupata majibu; tukifanya hivyo bila shaka lawama na manung’uniko yataisha. Na tutajikuta tunawajibika na kujituma kwa kutumia mbinu halali na njia halali ya kufikia jibu.


Tukigoma kujifunza, tunajiweka katika hali ya kutokua kiufahamu hususani kwenye kukabiliana na changamoto zinazotuzunguka.


Tunaweza kupata jibu la changamoto nyingi ikiwemo kutengeneza hela kihalali bila kutumia njia za mkato pale tu tunapojua, awamu hii na muhula huu, unahitaji mtanzamo mpya katika utatuzi wa matatizo yanayotuzunguka.
Na utatuzi unapofanyika, maana yake njia ya kufikia jibu inatakiwa kuwa wazi ili mtu yeyote anaekagua namna mwanafunzi alivyopata jibu, bila maswali ya ziada aone jibu lilivyopatikana.


Ili tufaulu hisabati za mwl. Magufuli hatuna budi kumpenda na kumkubali kuwa ndiye mwalimu wetu na tunawajibika kukubaliana na mbinu zake za kufundishia na kujifunza ili kupata matokeo tunayotarajia.


Wataalamu wa saikolojia wanaonesha kuwa, wanafunzi hufaulu vyema pale wanapokuwa na uhusinaano mzuri na mwalimu huhusani kwa kumpenda na kushirikiana nae hata nje ya saa za darasa kwa kwa nia njema ya kujifunza ili kutatua mafumbo kwa lengo la kupata majibu.


Chuki kwa mwalimu hupelekea kuchukia somo vilevile, na hatimaye kushindwa kukabili changamoto za masomo. Ufaulu wa masomo ni faida ya mwanafunzi kupata daraja zuri au alama nzuri. Ufaulu wa kutatua changamoto zinazotuzunguka, sisi wanafunzi (Watanzania) ni wafaidika wa kwanza.


Hii yanikumbusha siku chache zilizopita nilipata kuhudhuria mafunzo yaliyokuwa yakifanywa na maafisa wa kijeshi. Moja ya kitu nilichopata katika mafunzo yale, ni namna wapiganaji hao wanavyofikiri ili kupata majibu ya utatuzi wa maswali magumu au changamoto mbele yao.


Afisa mmoja akatoa mfano, ukikutana na mto wenye mamba wakali na unatakiwa kuvuka upande wa pili wa mto; Je utapita katikati ya maji ili mamba wakutafune au utafanya nini. Afisa yule wa kijeshi akaweka wazi kuwa, kuna namna ya kuishughulisha akili ili kupata suluhisho la kusonga mbele na kuendelea na safari ili kufika kule unakotaraji.
Moja ya suluhisho lililotolewa na mpiganaji yule ni kurusha kamba upande wa pili wa mto na kuifunga kamba nyingine kwenye kipago au mti mubwa na kisha kuvuka kwa kutambaa kwa miguu na mikono kwenye kamba huku mamba wakikukodolea macho unapopita juu yao.


Kwa mtu mwingine angeweza kurudi alikotoka, mwingine angeweza kutupa lawama ooh… kuna mamba kwenye mto, na mie siwezi kuvuka. Tofauti ya kufikiri kwenye tatizo lile lile ndilo linawafanya Wanajeshi kujiona washindi na akili zao zimejiengwa kusonga mbele hata pale mambo yanapokuwa magumu. Hivyo kurusha kamba upande wa pili na kisha, anavuka kwa kamba ni moja ya mbadala katika mbinu mpya ya kutatua tatizo la mto wenye mamba.


Katika nyakati hizi, tuna wajibu wa kufikiri kwa kiwango sawia na muongozo wa somo la awamu ya 5. Moja ya assignment (homework) aliyoitoa mwalimu Magufuli wakati mmoja akiongea na wahariri, ni waandishi kufungua kampuni ili kujenga viwanda au kuwa na shughuli ya uzalishaji mkubwa unaotoa ajira kwa vijana na kuongeza thamani ya malighafi hasa za mazao ya kilimo na mifugo. Nae Mheshimiwa Rais alitoa ahadi ya kusaidia mchakato ili kampuni hilo lipate mkopo kutoka benki ya ukekezaji. Je kuna, mtu au waandishi wameshapeleka andiko la mradi wa kampuni na mwalimu wetu wa darasa la awamu ya 5 akashidwa kutoa msaada? Au ndiyo wengi wanatumia kalamu na keyboard za social media kulalamika tu?


Kumbe tunaweza pia kungusha mti na kuulaza upande mmoja wa mto kwenda upande mwingine na kuvuka kwa kutambaa juu ya gogo la mti na kuendelea na safari ya maisha pasi kulalamika kwanini mwalimu anatuelekezea njia ngumu za kupata matokeo.


Mungu ibariki Tanzania. Tuna jukumu la kumkubali mwalimu wetu ili tufaulu mitihani katika zama za mafunzo mapya ili kupata alama nzuri na kusonga mbele katika hatua ijayo.


Fred Matuja

fmatuja@hotmail.com

No comments: