Tafuta/Search This Blog

Tuesday, March 10, 2009

Tunaelekea wapi?

Wananchi wenye hasira pamoja na polisi wakimtoa nje mtuhumiwa!!

Rais mstaafu,Ally Hassan Mwinyi,leo alikumbwa na jambo ambalo hakuna aliyelitegemea. Mwinyi alikuwa akihutubia wakati wa sherehe za Maulidi zilizofanyikia Diamond Jubilee. Punde si punde akatokea jamaa na kumchapa kibao. Kwa mujibu wa watu walioshuhudia kitendo hicho,kibao kilikuwa cha kushtukiza kwani kila mtu alidhani kijana huyo alikuwa anakwenda kumsalimia Kaimu Mufti Sheikh Suleyman Gorogosi aliyekuwa pembeni ya Mzee Mwinyi. Wengine walidhani kijana ni fundi mitambo na hivyo alikuwa anakwenda kurekebisha kipaza sauti. Tofauti na mawazo ya wengi,kijana huyo aligeuza mkono ghafla na kumnasa kibao Mzee Mwinyi. Kijana huyo ambaye ametambulika kwa jina la Ibrahim Said ana umri wa miaka 26.
Kabla ya kitendo hicho,Mzee Mwinyi,kama ambavyo amekuwa akifanya mara kwa mara,alikuwa akiwaasa waliohudhuria baraza hilo la Maulid kuepukana na ngono zembe kitu ambacho kinachangia sana kuenea kwa ugonjwa wa ukimwi.

Baada ya hapo jamaa alitolewa nje na walinzi wa Mzee Mwinyi wakisaidiana na waumini huku akipewa kichapo cha nguvu kama inavyoonekana pichani. Baada ya kutolewa nje kijana huyo, Mzee Mwinyi alisimama na kuwahakikishia waliokuwepo kwamba yupo fiti na shughuli inaweza kuendelea!

Pamoja na hayo maswali kadhaa yameshazuka kuhusu jamaa wa usalama. Walikuwa wapi? Na je nini kilipelekea kijana huyo kufanya alichokifanya? Ni maneno yaliyokuwemo kwenye hotuba ya Mzee Mwinyi? Je kijana ana matatizo ya akili? Pole sana Mzee Mwinyi.
Picha kwa hisani ya Dr.Faustine.
Habari na picha kutoka Bongo Celebrity.

No comments: