Tafuta/Search This Blog

Thursday, September 26, 2013

Rais Kagame aongeza sauti yake kwa wakosoaji wa ICC

Rais Paul Kagame wa Rwanda, leo ameongeza zauti yake kwa zile za viongozi wa Afrika ambao wameishutumu mahakama ya kimataifa ya uhalifu, ICC, kwa kuwalenga tu viongozi wa Afrika.
Katika hotuba yake kwenye mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Jumanne mchana, Bwana Kagame amesema Waafrika waliunga mkono muafaka wa kimataifa wa kuhakikisha wahalifu wanawajibishwa, na kubuniwa kwa mfumo wa kimataifa wa sheria wa kukabiliana na uhalifu kama huo, wakiamini kuwa mfumo kama huo ungeendeleza amani na usalama ndani na baina ya nchi, na kuendeleza usawa wa uhuru wa nchi zote. Badala yake, Bwana Kagame amesema mahakama ya ICC imekiuka malengo hayo.
ICC imeonyesha upendeleo ulio dhahiri dhidi ya Waafrika, badala ya kuendeleza haki na amani. Imelegeza juhudi za maridhiano, na kutumiwa kuwadhalilisha Waafrika na viongozi wao, pamoja na kuhudumia haja za kisiasa za wenye nguvu. Hakuna mahali ambako dosari ya ICC imeonekana zaidi kuliko katika kesi inayoendelea ya viongozi wa Kenya. Watu wa Kenya wameonyesha hamu ya kuponya vidonda vya zamani, kuridhiana na kwenda mbele. Ndio maana waliwachagua viongozi wao wa sasa wanaojibu mashtaka.
Rais Kagame amesema juhudi za maridhiano ya kijamii na kuendelea zinatakiwa ziungwe mkono, pamoja na juhudi za taasisi za kitaifa kukabiliana na uhalifu, badala ya kudhoofisha juhudi za kuziimarisha taasisi hizo. Amelitaka Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na Baraza la Usalama kulizingatia suala hilo na mengine yanayohusiana na sheria za kimataifa, ambayo tayari yamewasilishwa kwao, ili kudumisha haki, usawa wa kimataifa, kuunga mkono juhudi za maridhiano na kuheshimu utu wa Waafrika.

Habari kwa hisani ya Radio.un.org/sw  

No comments: